Friday, April 15, 2016

Zifahamu Sumu Kumi(10) Zinazowatesa Vijana Kwa Sasa.

Habari za wakati huu ndugu msomaji wa makala za mtandao huu, ni matumaini yangu kuwa hu mzima na unaendelea vizuri. Mimi pia naendelea vizuri katika harakati za kupambana kimaisha. Leo nakuletea mambo kumi ambayo kwangu nimeyaita sumu ambazo zinatukumba vijana wengi sana kwa sasa.




1. Kupenda starehe kuliko kazi,hili ni tatizo ambalo limekuwa likitukumba wengi sana kwa sasa. Leo hii kumekuwa na wimbi kubwa la vijana wengi sana ambao wanataka wao wastarehe tu siku zote ambapo mambo haya hayawezekani. Yaani huwezi kuishi kwa starehe siku zote, na kingine tulichosahau vijana ni kuwa starehe huja baada ya kazi lakini sisi kazi hatutaki kufanya ila tunachotaka ni starehe tu. Kwanzia leo acha hii tabia ya kupenda starehe kuliko kazi.

2. Kupenda kupewa kuliko kutoa, unapokuwa unataka kupewa jiulize wewe umetoa nini. Maisha ni kitu ambacho kina kanuni zake bhana, maisha sio kitu cha kukurupuka tu bali ni kitu ambacho kinahitaji kujipanga sana. Hivyo kama unapenda kupewa kumbuka na wewe kutoa. Usiwe mtu wa kutaka tu kupewa wakati wewe hutaki kutoa. Kuna mambo mengi ndani ya kutoa hivyo anza leo kutoa na kupokea kutakuja baadae.

3. Kufikiri siku zote wazazi watakuwepo,huu ni mkondo wa mawazo ambao ni mbovu kuishi ni kama wazazi watakuwepo siku zote ni kujidanganya sana. Jijengee uwezo wa kujitegemea mwenyewe sio kuwategemea wazazi kila siku.

4. Kudhani kuna njia za mkato, wengi sana tumekuwa tukijidanganya kuwa maishani kuna njia za mkato jambo ambalo ni kujidanganya sana, maishani hakuna njia ya mkato hivyo acha kujidanganya kwanzia sasa.

5. Tamaa ya mambo tusiyoyaweza au tusiyo na uwezo nao kwa wakati husika, vijana tumekuwa na taama za mambo ambayo hayana msingi wala umuhimu mkubwa sana maishani mwetu. Jifunze leo kufanya mambo ya maana. Pia jifunze kuepuka tamaa ya mambo usiyoyaweza.

6. Kuto kuwa na makundi sahihi, vijana wengi sana tumekuwa hatuna makundi sahihi, yaani makundi tuliyonayo sio ya kutujenga bali ni ya kurudisha nyuma zaidi na zaidi. Leo hii utakuta kijana anataka kuwa labda mtu fulani lakini makundi aliyonayo hayawezi kumfanya akafanikiwa. Nacho maanisha hapa ni marafiki ambao hatuendani.

7. Kuamini kuwa, kuwa na masters PhD au degree ndo kuwa na pesa, kuna wengi ambao tunaamini kuwa maishani kuwa na elimu za juu ndio kufanikiwa. Yaani ndio kuwa na pesa na mengineyo. Lakini maishani ukweli ni kuwa unauwezo wa kufanikiwa hata kama haukusoma kabisa. Hivyo basi futa hiyo imani yako.

8. Kuamini kuwa kujifunza au kusoma kunaishia vyuoni basi, vijana wengi sana tumekuwa tukiamini kuwa pindi tumalizapo elimu zetu za darasani basi ndio mwisho wa kujifunza. Huku ni kujidangaya na ndio maana tumekuwa hatufanikiwi. Hivyo kuanzia leo achana na habari hizi bali wewe endelea kujifunza hata baada ya kumaliza elimu yako ya darasani.

9. Kudhani kuwa na simu Kali ndio ufahari na utajiri, kila mtu leo hii anapigania kuwa na simu kali sijui iphone ngapi, sijui tecno gani n.k. huu ni ufahari kwa wale ambao hawajisomi lakini sio kwako wewe unayeyataka mafanikio. Kuwa na simu ya gharama ambayo haikusaidii kitu haina maana yoyote katika maisha yako.

10. Ujuaji hata kwa tusiyoyajua, tabia ya kujikuta unajua kila kitu inaponza maana hata kwa yale ambayo hujui wewe unajidai unajua, sasa hii wakati mwingine inakunyima fursa ya kujifunza maana wewe unahisi kuwa unajua kila kitu utajifunzaje sasa. Hivyo achana na tabia hii ambayo haifai.
Hizi ni sumu ambazo nimekuwekea kazi ni kwako kuendelea nazo au kuachana nazo, kila kheri.

Mwandishi: Baraka Maganga.
Mawasiliano:-simu-0754612413/0652612410.
                                                      :-barua pepe -Bmaganga22@gmail.com


1 comment: