Wednesday, January 6, 2016

Mambo Nane (8) Muhimu Ya Kukusaidia Katika Kubadili Tabia Yako Na Kuwa Mwenye Mafanikio

.
Habari ndugu msomaji wa mtandao huu wa kona ya maarifa, ni matumaini yangu kuwa unaendelea vizuri katika kuhakikisha kuwa unashughulikia ipasavyo yale unayo yahangaikia ili tu kujiletea mafanikio ambayo ndio kila mtu anayoyahangaikia. Nami nikusihi kwa moyo mmoja kuwa endelea kupambana mpaka uyatimize yale unayoyaamini kama mafanikio kwako. Pambana pambana bila kuchoka na mafanikio utayaona tu.
Wakati unaendelea kupambana katika kuhakikisha kuwa unafanikiwa ni vyema ukatambua kuwa yafuatayo ni mambo nane ya msingi ambayo yatakusaidia kuweza kubadili tabia yako ambayo pengine umekuwa huipendi na kuwa chanzo cha kuanza ile tabia ambayo unataka kuwa nayo na amabya unaamini kuwa itakuletea mafanikio. Mambo hayo ni yafuatayo:-





 Angalia yale mambo chanya tu, kama unataka kubadili tabia yako na kuifanya tabia yako iweze kukusaidia katika mafanikio, basi anza kuangalia mambo yako unayoyafanya katika upande chanya. Achana na mambo hasi katika maisha yako kwa kuwa mambo hasi hayajengi hata kidogo. Hivyo basi kwa kutambua hilo anza kutazama mambo chanya pekee maishani mwako.

2.    Jenga hali ya kufanya sasa, kama unatatizo la kuhairisha mambo na unataka kubadili tabia hii basi anza mara moja tabia hii ya kufanya sasa. Usiwe mtu wa kujiwekea vipolo vingi kuwa ntafanya baadae ntafanya baadae badala yake kuwa mtu wa kufanya pindi tu jambo hilo linapotakiwa kufanywa. Hii itakusaidia kuepuka ile tabia ya ntafanya baadae au ntafanya kesho matokeo yake unajikuta unarundo la shughuli nyingi sana.


3.    Jenga tabia ya kushukuru, je unajua kuwa neno shukurani ni neon muhimu sana katika kufanikiwa kwako, anza siku yako kwa kushukuru, mshukuru mungu kwa kukuamsha salama salimini, na kwa mengine mengi anayokutendea. Washukuru ndugu, jamaa na marafiki kwa kuwa nawe hata kama sio wakati wa shida au pale tu wanapotokea kukusaidia bali washukuru tu hata kwa kukupatia muda wa kuwa karibu nawe. Jifunze kushukuru na mengi utayaona ndani ya kushukuru.

4.    Jenga misingi ya program za kujifunza mwenyewe, kama ulikuwa na tabia ya kusubiri mpaka kila kitu ufundishwe sasa ni wakati wa kuacha na badala yake jenga tabia ya kuanza kujifunza mwenyewe. Kwa sasa dunia imebadilika, taarifa zipo sehemu nyingi sana hivyo huitaji kusubiri kila kitu badala yake fanya kutafuta taarifa za yale unayoyataka. Unaweza kujifunza juu ya yale unayoyataka kupitia blog kama hii, na nyingine nyingi zenye kufanana nah ii, pia unaweza kujifunza kupitia google, vitabu, majarida na vipeperushi mbalimbali.


5.    Jenga heshima binafsi, kila mtu lazima ajiheshimu kwanza ndipo naye atapaswa kuheshimiwa, kama unakumbwa na kauli mbaya kama zile za mtu mzima ovyo au mtu mzima alafu hujiheshimu, basi ni wakati sasa wa kuamua kujijengea heshima binafsi ili iweze kukusaidia kuweza kuonekana kuwa mtu bora na mwenye kutegemewa na jamii. Anza kujifunza namna ya kuanza kujiheshimu mwenyewe ili nawe uheshimiwe. Heshima itakupa nafasi na kukufungulia mlango wa kushirikiana na watu mbalimbali.

6.    Epuka vishawishi vyote hasi, kama kweli umeamua kubadili tabia hasi basi ni wakati sasa wa kuchukua hatua nyingine muhimu ambayo ni kuepukana na vishawishi vyote vyenye kuleta tabia hasi. Kama unahisi marafiki zako ni chanzo cha tabia zako hasi ni wakati wa kuachana nao sasa na kutafuta marafiki wapya.


7.    Jifunze kuyapenda yale unayotakiwa kuyafanya, kama unatabia ya kuchukia yale unayoyafanya sasa ni wakati na fursa nyingine kwako kubadili tabia hii na badala yake anza kwa kupenda yale unayoyafanya. Hii ndio tabia muhimu ya mtu anayetaka kufanikiwa. Hii ni kwa kuwa mtu anayetaka kufanikiwa lazima akipende kile anachokifanya ndipo atayaona mafanikio, kinyume na hapo hawezi. hivyo basi kwa kulitambua hilo jenga basi hiyo tabia ya kupenda unalolifanya.

8.    Anza siku mpya kwa kitu chanya, hapa unatakiwa unapoamuka kwanza amka na fikira chanya badala ya kusema siku mbaya sema hii ni siku mpya, nzuri ambayo mungu kanipatia ili niweze kufanya yale nayotaka kuyafanya na kuyatimiza. Anza siku yako kwa kauli zenye kutia nguvu na kukujenga kiakili na kifikira.

Mambo hayo nane ni muhimu uyafuatilie kwa makini kama kweli unataka kubadili tabia yako na kuwa mwenye mafanikio makubwa maishani. Yafanyie kazi haya.

Ni mimi rafiki yako,
Baraka Maganga
Wasiliana nami kwa.
 Simu: 0754612413 au 0652612410.
Barua pepe: Bmaganga22@gmail.com


No comments:

Post a Comment