Tuesday, April 5, 2016

Fahamu Kuwa Kila Jambo Linatawaliwa Na Kitu Hiki


Duniani kuna vitu vingi sana ambavyo binadamu huwa tunakuwa tunavifanya au tunataka kuvifanya, vitu hivi vinaweza kuwa vizuri au vibaya kutoka kwa mtu mmoja mpaka mtu mwingine hii ni kutokana na tofauti za kimtazamo miongoni mwetu binadamu. Lakini pamoja na tofauti hizi za kimtazamo huwa tunakuwa na kitu kimoja ambacho kinaweza kutuunganisha na kutuweka pamoja na kitu hiki ndicho ambacho wapaswa kujua na kwenda nacho kama unataka kupata matokeo makubwa. Kitu hicho sio kingine bali ni kanuni.

Nafahamu kanuni sio jambo geni sana kwako ndugu msomaji. Kwa wale ambao wamebahatika kupita katika shule kuna masomo kama hisabati na fizikia mfano haya ni masomo yenye kutawaliwa na kanuni, yaani katika utafutaji wa majawabu ya maswali ya hesabu kuna kanuni na ukienda kinyume na kanuni hiyo hauwezi kupata jibu mwafaka la swali lako. Mfano katika hisabati kuna kanuni maarufu sana ijulikanayo kama MAGAZIJUTO. Hii kanuni ni kifupi cha baadhi ya matendo mfano MA- husimama kwa niaba ya mabano wakati GA- husimama kwa niaba ya gawanya. Hivyo katika kufanya swali la mtindo huu lazima uanze na kuzitoa namba katika mabano, uje ugawanye, baadae uzidishe, ujumlishe na hatimaye utoe. Hivyo ndivyo kanuni isemevyo na kwa kufanya hivyo basi utapata jibu sahihi kinyume na hapo hupati jibu.


Sasa kama ilivyo katika hesabu hata katika maisha halisia haya mambo yako hivyo hivyo. Maishani kila kitu kina kanuni zake leo hii ukitaka kulima nyanya, kilimo hiki cha nyanya kina kanuni zake, ambazo lazima uzifuate kwa makini na kama inavyotakiwa ndipo utapata mazao bora. Ukitaka kulima miti lazima ujue kanuni za miti, mfano miti mingi huwa tayari kwa kuvunwa baada ya kipindi cha miaka kuanzia mitano na kuendelea hiyo ni kanuni ambayo unatakiwa uifuate kinyume na hapo hauwezi kupata kitu chochote kutoka katika miti. Kwahiyo katika kilimo mfano jambo nalo taka kusisitiza ni kuwa kila zao lina utaratibu wake ambao ni muhimu sana kwa nza sio muhimu ni lazima ufuatwe na anaefanya kilimo husika, na ikumbukwe kuwa tofauti za mazao zinaleta tofauti za kanuni ndio maana kanuni za miti huwezi kupeleka kwenye nyanya au pilipili hoho.

Mafanikio ni kitu ambacho kina kanuni nyingi sana tena sana, mfano wa kanuni hizo ni kama vile jiwekee malengo, usikate tamaa, kuwa na marafiki chanya, fanya mazoezi ili kuimarisha afya ya mwili wako, tafuta timu sahihi ya kushirikiana nayo, kuwa mvumilivu, ua hofu,kuwa na msimamo,epuka visingizion.k.

Pengine umezoea kanuni haziko katika maandishi yaani umezoea kanuni huwa zinakuwa katika mfumo wa namba, sikulaumu hii ni kutokana na mfumo wa elimu ambao umepitia ambapo kila kanuni huwa ipo katika mfumu wa namba, lakini kumbuka kuwa kule ni shuleni na hapa tunazungumzia maisha halisi hivyo sio lazima kanuni hizi ziwe katika mfumo wa namba. Katika maisha halisi kanuni nyingi zipo katika mfumo wa maandishi na ninaposema kanuni simaanishi mtu mpaka uambiwe hii ndio kanuni hapana bali nacho rejelea hapa ni ile hali hata ya kupewa utaratibu au maelezo ya jinsi gani ya kulifanya jambo hicho ndicho nacho maanisha napo sema kanuni.


Swali la kujiuliza leo ni kuwa je unazijua kanuni za unachokifanya? Kama jibu ni ndio je unazifuatata? Kama hauzifuati basi nakuambia leo hiyo ndio sababu namba moja ya kwanini haufanikiwi. Na kama huzijui unasubiri nini? anza kuzitafuta kuanzia leo hii.

Mwandishi: Baraka Maganga.
Mawasiliano:-simu-0754612413/0652612410.


No comments:

Post a Comment