Monday, February 15, 2016

Jifunze Na Jua Kwamba Kuna Muda Unatakiwa Kusema Hapana.


Habari za wakati huu ndugu mpendwa msomaji wa makala za mtandao huu, ni matumaini yangu kuwa hu mzima wa afya na unaendelea vizuri
kwa kiasi kikubwa sana. Ni matumaini yangu kuwa unaendelea kupambana ilivyo katika kuhakikisha kuwa unatekeleza malengo yako kwa kiwango kikubwa zaidi nami nikusihi kuwa endelea kupambana maana ni muhimu ukayatimiza malengo yako na hapo ndio utaona maana ya kuishi.






Je ulishawahi waza juu ya umuhimu wa kusema hapana? Nataka nikuambie ndugu msomaji wa makala hii kuwa kuna muda unatakiwa useme hapana katika maisha yako kama ulikuwa huna tabia hii basi anza kujifunza kwanzia leo kuwa unahitaji kusema hapana muda mwingine usiwe mtu wa ndio kwa kila jambo bali tambua kuwa kuna mazingira unahitajika kusema hapana katika maisha yako. Lazima uishi huku ukiamini kuwa kuna wakati unahitajika kusema hapana tena kwa nguvu zako zote sema hapana hapana.

Kuna wakati itafika utakuwa unafanya jambo fulani mara ukapatwa na hali fulani ya kutaka kukata tamaa, sasa ukijikuta umeanza kufanya jambo fulani alafu ukaijiwa na halli fulani ya kutaka kukata tamaa hapa ndipo sasa unatakiwa useme hapana, hapana sito kata tamaa. Na utakaposema hapana utajikuta unaendelea kutenda zaidi na unapata matokeo uliyokusudia. Kuna stori ya jamaa mmoja ambaye alishindwa kulitunza shamba lake na hivyo kutokana na sababu zake kadha wa kadha wazo la kuliuza likamwijia na kwa kuwa alishindwa kujizuia kusema hapana akajikuta ameuza kumbe shamba lile aliloliuza lilikuwa na madini ya kutosha na aliyenunua akawa billionea. Hivyo unapohisi unataka kukata tamaa sema hapana na endelea mpaka upate matokeo uliyokusidia.

Kuna wakati unajikuta unafanya mambo kisa umeambiwa na watu ambao wanakuzidi umri mfano kaka yako, baba, mama, au dada, bibi au babu. Sisemi kuwa uwapinge ila nachotaka kukuambia kuwa wakati mwingine unatakiwa kusema hapana kwao maana mitazamo yao inaweza kuwa hasi yenye kukuangamiza lakini wewe ukaamua kuifuata na kuishi nayo. Mfano ndugu zako wanakuambia kuwa si unaona sisi ni masikini hivyo katika ukoo wetu hakuna anayeweza kuwa tajiri wewe sema hapana mimi naweza kuwa tajiri usikubali kila kitu.
Njoo kwenye mahusiano ni mara ngapi watu wamekuwa wakifanya mambo ya ajabu tena ya kipuuzi na yasiyo na maana ili tu kuwaridhisha wapenzi wao. Watu wako tayari kuwadharau hata wazazi wao kuwasaliti ndugu zao kisa wapenzi wao na hii ni katika kuwaridhisha tu wapenzi wao na kuonyesha kuwa wanawajali au kama njia ya kulinda mahusiano yao, mfano mpenzi wako wa kiume anakuambia toroka kwenu leo usiku uje kwangu wakati wewe unajua kuna hatari ya wewe kushitukiwa hata kabla ujatekeleza hilo jambo, jifunze kusema hapana kwa mpenzi wako muda mwingine.

Marafiki wanakushawishi kunywa pombe ili hali wewe unajua pombe ni mbaya na madhara yake mengi unayajua lakini eti kisa kuwaridhisha rafiki zako unakubali kunywa pombe na hatimaye kuwa mlevi wa kupindukia na kujikuta unakuwa na maisha mabovu kisa ulevi wako huo, kwanini hausemi hapana kwa  rafiki yako, jifunze kusema hapana kwa marafiki wenye kukushawishi wewe kufanya mambo usiyoyataka kwa kiwango kikubwa usihofie kuvunja nao mahusiano.

Kusema hapana sio utovu wa nidhamu na wala sikufundishi wewe kuwa mtovu wa nidhamu bali nataka uwe na uwazi na ukweli wa kusema hapana wakati mwingine sio unakubali kubali kupelekwa na watu au hali fulani ya kimaisha au mwili wako.

Ni mimi rafiki yako,
Baraka Maganga.
Wasiliana nami kwa nambari za simu 0754612413/0654612410 au kwa barua pepe:- Bmaganga22@gmail.com.


No comments:

Post a Comment