Friday, January 15, 2016

Huwezi Kufanikiwa Kama Utashindwa Kuepuka Jambo Hili.

Habari za wakati huu ndugu mpendwa msomaji wa makala za mtandao huu wa kona ya maarifa, ni matumaini yangu kuwa hu mzima wa afya na unaendelea vizuri katika kuhakikisha kuwa unayatekeleza yale ambayo umepanga kuyatekeleza. Vizuri endelea kupigana mpaka yale unayoyataka yamekamilika.





Wakati unaendelea kupambana, ili kuhakikisha kuwa unayatekeleza yale unayoyataka basi nakusihii epuka kitu hiki kimoja kama kweli unataka kufanikiwa katika maisha yako.jambo lenyewe ni kukosa ubunifu. Nimeamua kukuandikia hili ndugu msomaji ili uweze kuelewa madhara ya jambo hili. Na hili nimeamua kuliandika kutokana na ongezeko la tabia hii miongoni mwa watu wengi, na watanzania tukiwa ndio tunao ongoza kwa tabia hii ambayo kwangu naiona kama tabia isiyofaa kabisa kuigwa wala kufuatwa na jamii.


Tabia yenyewe ni ya kukosa ubunifu miongoni mwetu. Ukitazama shughuli nyingi sana za watanzania ni shughuli ambazo zimwekosa ubunifu, kabisa angalia sanaa zetu, biashara n.k, ni shughuli chache sana zenye kubeba ubunifu ndani yake. Watu siku hizi hawaangaiki kubuni kitu chochote badala yake wamekuwa ni watu wa kuhamisha mambo kama yalivyo kutoka walikoyatoa na kuyaleta kwetu,(coping and pasting), na kwa kuwa watu pia ubunifu umewapiga chenga basi nao huwa wanakubali kuamini mambo hayo hata kama wanajua hayaendani na sisi. Kutokana na ukosefu wa ubunifu ndio maana leo hii kumekuwa na tabia kubwa sana ya mambo ya kuigana igana tu na matokeo yake hakuna jipya linalo fanyika bali ni yale yale.


Ikiwa unataka kufanikiwa katika dunia ya leo basi hakikisha kuwa unakuwa mbunifu. Dunia ya leo imejaa ushindani wa hali ya juu, hii ikimaanisha kuwa kwa kila unalolifanya unaweza usiwe peke yako badala yake mtakuwa wengi. Sasa kama ikitokea mmekuwa wengi basi jambo la msingi la wewe kufanya ni kutafuta namna ya pekee ya kuweza kulifanya jambo lile ambalo litakutofautisha wewe na wengine. Kama ukishindwa kufanya hivyo basi tambua kuwa hautopata mafanikio makubwa katika yale unayoyafanya.


Chukulia mfano wa wachezaji Ronaldo na Messi, unajua ni kwa nini wanakuwa wachezaji bora wao tu kuliko wengine?, je wao ndio wachezaji pekee duniani kwamba hakuna wenzao. Ukiwaangalia wao kama wao hawana tofauti na wachezaji wengine maana wao wana miguu miwili kama wenzao wapo watu duniani ambao wanacheza namba kama zao lakini nini kinachofanya wao wafanikiwae kuliko wenzao, hakuna kingine bali ni ubunifu ambao wanao. Ubunifu wao ndio unawatofautisha wao na wenzao na kuwafanya waonekane bora kuliko wao. Wote wanafunga magoli, wanapiga chenga na bwebwe zingine zote unazozijua katika mpira lakini nini kinawatofautisha na wengine? Ni ubunifu walio nao ndio maana unakuta wanamagoli mengi kuliko wenzao. Wamebuni mbinu tofauti za kucheza mpira ambazo wenzao hawana muda wa kuzibuni ndio maana wanakuwa bora.


Tukirudi katika biashara za hapa kwetu Tanzania, ni biashara bora kwa kiasi chake lakini ni biashara ambazo zimejaa maswala ya kuigana tu hakuna jipya. Leo hii kumezuka maswala ya biashara za mtandao sasa kila mtu anataka afanye, achilia mbali maswala hayo, kutokana na maendeleo ya watu kutumia mitandao ya kijamiii watu wamekuwa na uwezo wa kutangaza biashara zao katika mitandao hiyo, lakini angalia namna ya utangazaji wao, kila mtu anapiga picha ya bidhaa na kuipost kisha ataandika tu kwa anae hitaji mawasiliano haya hapa, anatoa namba yake pale. Kama  sio hivyo utasikia, jipatie laba kali, tisheti n.k tunakuletea ulipo. Sasa biashara hizi sio kuwa nazipinga au kuwacheka wanaozifanya lakini nalo hoji ni kuwa ni lazima wote tuandike matangazo sawa hakuna anaeweza kubuni namna nyingine ambayo itamtofautisha na mwingine.


Angalia leo kuna makundi kibao katika mitandao mbalimbali makundi haya huanza kwa namna nzuri sana lakini kutokana na kuwa wote tumeathiriwa na namna moja ya kufikiri na hivyo tukakosa ubunifu, utakuta mtu kaanzisha kundi kaliita jina la kibiashara kabisa lakini ukiingia kwenye kundi hilo unakutana na stori za mapenzi, kwa kuwa ameona kuwa stori hizo ndizo zinazopendwa na kufuatiliwa na kuwapatia watu wengi sana umaarufu mkubwa. Angalia leo hii ni makundi mangapi yanazungumzia mapenzi, hakika yatakuwa mengi sana na yote yanaandika kitu kile kile hii inaonyesha kuwa hatuna ubunifu wa kutuwezesha watu  kuweza kufanya kitu cha tofauti.


Kimsingi ni vyema ukatambua kuwa katika dunia ya sasa, yenye kujaa ushindani wa hali ya juu huitaji kufanya kitu cha tofauti sana ila unatakiwa ufanye kitu kwa utofauti na hiyo ndio tabia ya watu walio fanikiwa. Sio kuwa wanafanya vitu tofauti bali wanafanya vitu kwa utofauti, na utofauti huo ndio ujulikanao kama ubunifu.  Na ndio huwafanya waonekane watu wa tofauti sana duniani.


Ni mimi rafiki yako,
Baraka Maganga.
Wasiliana nami kwa.
 Simu: 0754612413 au 0652612410.
Barua pepe: Bmaganga22@gmail.com.


No comments:

Post a Comment