Thursday, December 3, 2015

Hili Ndilo Kosa Ambalo Wengi Hulifanya.


Habari za wakati huu ndugu msomaji wa mtandao huu wa kona ya maarifa, ni matumaini yangu kuwa hu mzima wa afya na unaendelea vizuri katika mapambano yako na kuhakikisha mwisho wa siku unafika kule ulikokuwa unahitaji kufika. Nami nasema usikatetama wala kurudi nyuma kwani mapambano yanaendelea.
Binadamu tumekuwa watu wa kufanya makosa mbalimbali, ambapo mengine huwa tunayatenda ama kwa kujua au kuto kujua. Yote kwa yote ni katika mfumo wa maisha kwa kuwa kuna usemi wa kiingereza usemao “we learn through mistakes and those who never commit mistakes they never learn” ukiwa na maana kuwa tunajifunza kupitia makosa na yule asiyefanya makosa hajifunzi. Nianzie hapa kauli imesema tunajifunza kupitia makosa hii haina maana kuwa ufanye kosa  makusudi alafu useme najifunza. Kauli hii haswa ipo kwa lengo la kutuhamasisha kuwa tuwe watu wa kujaribi tena tusiwe watu wa kuogopa kujaribu kisa tunahofia kushindwa au kufanya makosa maana tunajifunza kupitia makosa.
Ulishawahi kuambiwa kuwa fanya kitu fulani kisha ukatoa jibu kuwa siwezi bila hata kuthubutu kujaribu?, mara ngapi umekuwa ukiwasihi ndugu, jamaa, marafiki na watu wengine wa karibu nawe kuwa wafanye jambo fulani wakakujibu pale pale pasipo hata kufanya tathimini ya kile unachowaambia wakatoa jibu la kuwa hawawezi. Kauli ya siwezi imekuwa kauli maarufu na naiona ikishika kasi sana miongoni mwa watanzania. Na hili ndio kosa ambalo wengi tumekuwa tukilifanya ama kwa kujua au kuto kujua. Kama ulikuwa hujui hili ni kosa leo nakuambia hili ni kosa tena kosa  kubwa sana ambalo unalifanya. Unaweza kujiuliza kivipi si nasema ukweli kuwa siwezi kwa mambo ambayo naamini siwezi au mbona hili kwangu mimi najua haliwezekani ndio maana nimesema siwezi n.k. baada ya hapo ukaongeza na swali kuwa kivipi sasa nasema unafanya kosa?
Uchunguzi unaonesha kuwa miongoni mwa watu wengi wanaosema hawawezi ni wale wenye kukosa hali ya uthubutu yaaani ni wale ambao wao huogopa kufanya jambo fulani kisa tu wamejijengea imani kuwa hawawezi . Mafanikio huja kwa kuziona fursa na kuzitumia sasa kwa kuwa hauna  ule moyo wa uthubutu kila fursa inayokuja wewe unasema huwezi na matokeo yake unaendelea kubaki pale pale bila kufanya lolote zaidi unaendelea kujididimiza kwa kauli yako mbovu ya siwezi. Ki vipi unawezaje kusema hauwezi ikiwa haujajalibu jambo husika? Umewezaje kujua kuwa hauwezi kwa kukaa tu kuliangalia jambo bila kujihusisha nalo kisha ukasema aaa! Jambo hilo siwezi. Nimesema kuwa watu wanaopenda kutumia kauli ya siwezi ni wale wenye kukosa ile hali ya uthubutu yaani wao kwa namna yoyote ile huwa hawataki kujaribu mambo, wao hukaa tu na kusema hawawezi.
Naamini wewe unayesoma makala hizi na kunufaika nazo umeweza kufanya hivyo kwasababu ulithubutubu kujifunza kusoma na pengine kuandika, ndio maana leo hii unauwezo wa kusoma makala hii na nyingine nyingi. Sasa kama ulithubutu kujifunza kusoma na ukaweza na faida zake umeziona na unaendelea kuziona, sasa  kwanini leo hii linapokuja suala la fursa fulani unagoma kuifuata kwa madai kwamba hauwezi. Nani kakuambia huwezi?, Nani kakuaminisha kuwa hauwezi?, Unawezaje kusema hauwezi ikiwa haujajaribu jambo husika?,. Ukijiuliza maswali haya na jibu likawa sijui. Yaani hauna majibu ya ni nani alikuambia huwezi, uliamini vipi hauwezi ikiwa hujajaribu basi jua fika unajidanganya na kujipotezea muda wako.
Jambo la msingi ambalo inabidi ulifahamu ni kuwa akili ya mwanadamu hufanya kazi vizuri pale inapowekwa katika hali ya kufikiri juu ya changamoto zinazokukabili. Akili yako huamka na kuchemka kufanya jambo pindi unapojiuliza maswali kama kivipi ntafanya jambo hili, vile vile akili yako hulala pale ambapo hauifanyi ikafikiri juu ya changamoto zinazokukabili na ndio maana umekuwa bingwa wakauli za siwezi.
 Acha mara moja kutumia kauli ya siwezi hata kwa mambo ambayo hujajaribu, na hata kama ulijaribu ukashindwa wafuate wale waliofanikiwa katika jambo husika ili uwaombe ushauri pengine hautumii njia sahihi katika jambo husika ndio maana unashindwa.
Ni mimi rafiki yako,
Baraka Maganga.

0754612413/0652612410.

No comments:

Post a Comment