Monday, December 14, 2015

Anza Na Kitu Hiki Kimoja Kama Kweli Unataka Kufanikiwa.


Habari ya siku ndugu msomaji wa mtandao huu wa kona ya maarifa ni matumaini yangu kuwa hu mzima wa afya na unaendelea vizuri na majukumu ya hapa na pale, yote haya  ni katika kuhakikisha kuwa unapata kuyatimiza yale ambayo umekwisha kuyaweka kama malengo yako na  mwisho wa siku unapata mafanikio ambayo umekuwa ukiyatafuta kwa nguvu. Baada ya kuwa kimya kwa siku mbili tatu hivi kutokana na sababu ambazo ziko nje ya uwezo wangu, naomba tureje na kuweza kuendelea kupeana maarifa ya hapa na pale.
Katika makala ya leo nataka kukushirikisha juu ya jambo moja,Jambo lenyewe ni umuhimu wa kuanza kuheshimu vitu vidogovidogo. Nimeamua kuandika juu ya jambo hili ili kuweza kukunasua  katika mtego huu ambao unawaangamiza watu wengi. Ndugu msomaji wa mtandao huu nataka nikusihi kwamba kwanzia leo jenga tabia hii muhimu ambayo ni ya kuheshimu vitu vidogovidogo.

Nataka ujenge tabia hii kwa kuwa itakufanya ufanikiwe zaidi. Kwanini jambo hili litakuifanya ufanikiwe ni kwa sababu vitu vidogo ndivyo huwa vinavijenga vitu vikubwa. Chukulia mfano wa nyumba, nyumba haiwi nyumba bila msingi sasa kwa hesabu za kawaida ukichukulia kigezo cha ukubwa kimsingi,msingi wa nyumba ni mkubwa kuliko nyumba, lakini ukweli ni kwamba nyumba haiwi nyumba bila msingi. Hivyo ili ujenge nyumba lazima uanze na msingi bila msingi hakuna nyumba hivyo basi kwa kutumia mfano huu wa nyumba jenga tabia ya kuvithamini vitu vidogovidogo.





Leo hii kuonesha ni jinsi gani watu hawathamini vitu vidogo utamsikia mtu akikuambia siwezi kufanya biashara fulani kwa sababu nina pesa chache ambayo haiwezi kunifanya nianzishe biashara hiyo husika, leo hii watu wamekuwa wakisubiri kupata milioni kadhaa ndio waanzishe biashara zao hizo wanazo zifikiria, lakini cha ajabu ni kuwa wamekuwa wakisubiri kwa miaka kadhaa na wasipate hizo milioni za kuanzisha biashara zao husika. Kumbuka kuwa huwezi kufika kumi bila kuanza na moja. Hivyo kama unataka kufika kumi lazima upitie moja, mbili, tatu na kuendelea ndipo utafika kumi. Hivyo hata kama unataka kufanya biashar ya mamilioni anza hata na maelfu yatakuwa na baadae itafika hiyo milioni hakuna namna nyingine. Usiendelee kusubiri kupata milioni wakati hauthamini pesa ndogo ambayo itakufanya ufike kwenye mamilioni.
Kudharau vitu vidogovidogo kumewaponza watu wengi sana na kuwafanya wabaki pale pale na wasipige hatua yoyote ile ya kimaendeleo. Leo hii watu hawawezi kujiwekea akiba ya pesa,kwa kuwa hawathamini pesa ndogondogo. Leo hii mtu huona shilingi mia moja ni kama pesa ya kuchezea tu maana ni ndogo na hawezi kuifanyia chochote. Kama unatabia hii acha mara moja maana itakugharimu sio muda. Kuna msemo wa Kiswahili usemao “mazoea hujenga tabia”. Hivyo basi kama huwezi kuthamini pesa ndogo kama shilingi mia uwapo na wazo la elfu kumi,vivyo hivyo huto weza kuja kuithamini shilingi elfu kumi ukiwa na wazo la milioni, hii ni kwa sababu usha jijengea tabia ya kuto kuthamini vitu vidogo huko nyuma.
Wapo watu ambao wamevithamini vitu vidogo na matokeo yake wakapata mafanikio makubwa, kuna mifano ya watu ambao waliamua kuanzisha biashara zao wakiwa na mitaji midogo sana ambayo hata wakikuambia leo hii utawaona kama waongo wenye lengo la kukudanganya tu, lakini ukweli ni kuwa watu hawa walielewa umuhimu wa kuvithamini vitu vidogo ndio maana wakaamua kuanzisha biashara zao japo kuwa walikuwa na mitaji midogo na matokeo yake ni kuwa walifanikiwa sana maishani mwao, hivyo jifunze kupitia watu hao ambao wamefanikiwa.
Kama kweli unataka kufanikiwa basi jenga tabia ya kuvithamini vitu vidogo maana hivyo ndivyo huleta mafananikio makubwa kumbuka mfano wa punje moja ya mhindi ambayo hufukiwa ardhini na baadae huzaa punje nyingi ambazo hutumika kama chakula cha kuwasaidia watu.
Ni mimi rafiki yako
Baraka Maganga.

0754612413/0652612410.

No comments:

Post a Comment